Taught by
Stephen Armstrong
Taught by
Stephen ArmstrongNi wakati wa kuanza kujifunza kuhusu Ufalme wa Kristo duniani, ambao unafuata siku 75 baada ya kurudi Kwake Duniani.
Maandalizi yote yamefanywa kwa ajili ya Ufalme kuanza
Dunia imerejeshwa katika uzuri wake
Hekalu limesafishwa na kujengwa upya kwa namna mpya na bora zaidi
Uovu wa dunia umewekwa kando, angalau kwa muda
Na raia wa ufalme wako tayari kupokea urithi wao wakati huo
Watakatifu wote waliofufuliwa kutoka Agano la Kale, Kanisa na Dhiki wanaingia katika Ufalme
Pamoja na wale waamini ambao hawakufa katika Dhiki
Na wasioamini wote walio hai, ambao ni Mataifa pekee kwa wakati huu, wanapelekwa Hadesi (Kuzimu)
Kwa hiyo sasa tunaingia kujifunza kuhusu Ufalme.
Na tukigeukia kitabu cha Ufunuo ili kujifunza wakati huo, tutakatishwa tamaa sana na kile tunachokipata
Tukirejea pale tulipoishia, haya ndiyo tunayoyapata
Katika mstari wa 6 tunajifunza kinachotokea kabla ya ufalme kuanza, na katika mstari wa 7 tunajifunza kinachotokea baada ya ufalme kuisha.
Kwa hiyo kitabu cha Ufunuo hakituambii chochote kuhusu kile kinachotokea wakati wa miaka 1,000 ya ufalme
Kipindi chote cha ufalme kinafanyika kati ya mstari wa 6-7 katika kitabu cha Ufunuo
Kitu pekee ambacho kitabu cha Ufunuo kinatuambia kuhusu Ufalme ni urefu wa wakati huo: miaka 1,000
Sababu ya Ufunuo kupuuza kabisa maelezo ya Ufalme ni kwa sababu sehemu iliyobaki ya Biblia imejaa maelezo hayo.
Ufalme umeelezewa katika Torati na ni mada kuu ya manabii na Zaburi za Agano la Kale.
Yesu anatoa maelezo ya kuvutia katika mifano yake mingi na mafundisho mengine
Na hata waandishi wa nyaraka wanatupa maelezo machache
Kwa hiyo, tunalazimika kutoka nje ya kitabu cha Ufunuo kwa wiki mbili zijazo ili kuchunguza maisha na nyakati za Ufalme.
Tuanze kwa kukumbuka maana ya neno "ufalme" katika Biblia
Wakristo wengi hufanya kazi kwa uelewa mdogo sana na wa juujuu kuhusu mustakabali wao wa milele.
Dhana ya Ufalme (au Mbinguni) kwa kiasi kikubwa imepunguzwa hadi kwenye theolojia ya Hallmark - "theolojia ya kadi za pongezi".
Kwa hiyo, uelewa wetu kwa kiasi kikubwa hauna maana au kiini
Kwa kushangaza, Biblia inazungumzia kwa mapana kuhusu ufalme ujao kwa kutumia maneno mbalimbali, maelezo na picha au vivuli
Kwa kweli, Ufalme ujao ni mojawapo ya mada muhimu zaidi za Agano la Kale, wa pili kwa Masihi pekee.
Tunaweza kupata marejeo haya halisi kutoka Mwanzo hadi Malaki
Na katika Agano Jipya, mijadala kuhusu ufalme ilikuwa muhimu sana kwa huduma ya Yesu
Kuna marejeo 160 ya ufalme katika Agano Jipya na 125 yanapatikana katika Injili.
Yesu alizungumzia kuingia katika ufalme, kuishi katika ufalme, kutawala katika ufalme, na kuwa na urithi katika ufalme
Paulo pia alifundisha kwamba tungepokea urithi wetu katika ufalme Kristo atakaporudi
Na sasa Ufunuo umetueleza kwamba Ufalme utakuwa wa miaka 1,000.
Tukiangalia mafundisho ya Biblia kuhusu Ufalme katika marejeo haya yote, tunaona dhana ya Ufalme ikiendelea kukua
Dhana ya Ufalme hubadilika kupitia hatua nne za maana kutoka Agano la Kale hadi Agano Jipya
Na ni muhimu kutambua sehemu hizi za mpito ili kufikia tafsiri sahihi
Mada ya Ufalme inaanza katika Mwanzo kama ahadi, jambo ambalo Mungu angefanya ili kurekebisha dhambi ya Adamu
Ahadi hiyo imeelezwa waziwazi katika maagano ya Ibrahimu na Daudi
Taifa la Israeli lingefurahia urithi wa nchi, wazao wengi, mfalme mkamilifu na amani isiyo na mwisho
Na vizazi vingi vya waamini wa Israeli vilitarajia utimilifu wa ahadi hiyo ya baadaye.
Kisha wakati ukafika wa kutimiza ahadi hiyo, na Bwana akaja kwa Israeli akitoa Ufalme siku hiyo.
Yesu aliwapa Israeli pendekezo: mnipokee kama Mfalme wenu, nami nitawapa Ufalme ulioahidiwa.
Lakini Israeli walimkataa mfalme wao, kama tunavyojifunza katika Mathayo
Na matokeo yake, Yesu aliondoa pendekezo lake na Ufalme ukachukuliwa kutoka kwa kizazi hicho cha Israeli.
Katika nafasi yao, mwaliko wa Ufalme ulipewa Mataifa, ambao wakawa Bibi-arusi wa Kristo badala ya Israeli.
Kwa hiyo pendekezo la Ufalme likasitishwa kwa muda, na mahali pake likaibuka mpango wa kuwahusisha Mataifa ili kuingia katika Ufalme.
Mpango huu unaendeleza wito wa kumwamini Yesu, na mtu anapoitiki wito huo, anakuwa sehemu ya Ufalme wa kiroho.
Wanakuwa raia wa Ufalme wa mbinguni ambao si wa ulimwengu huu
Na mpango huu utaendelea hadi Bwana atakapouhitimisha kwa kumwita Bibi Arusi Wake Mbinguni wakati wa ufufuo.
Kisha kama tulivyojifunza, Bwana atarudi duniani mara ya pili, na wakati huo Ufalme utaonekana kama ulivyoahidiwa.
Wakati huo Ufalme utakuwa mahali halisi kama vile Mungu alivyomwahidi Ibrahimu na wazao wake
Ufalme huo utakuwapo duniani katika wakati ujao, na utawajumuisha wanaume na wanawake kutoka mataifa yote.
Hili pia ni utimilifu wa ahadi za Mungu kwa Ibrahimu, aliposema kwamba mataifa yote ya dunia yangebarikiwa kupitia kwake.
Kwa hiyo, wazo la Ufalme linaendelea kutoka kuwa ahadi, hadi kuwa pendekezo, kisha kuwa mpango, na hatimaye kuwa mahali halisi
KKatika hatua tuliyofikia katika Ufunuo, tumeona mpango huo ukifikia mwisho wakati wa kunyakuliwa kwa Kanisa.
Na sasa tunaona Ufalme ukianza wakati wa kuja kwa Kristo mara ya pili
Na katika wakati huu ujao, mambo yote mema ambayo Bwana amewaahidi watu wake hatimaye yatatimizwa.
Tunasubiri Ufalme ili tuone ahadi Zake zikitimizwa kwa sababu ahadi hizo ziliwekwa wakati huo, si wakati huu.
Kwa hiyo, sasa ni wakati wa kujifunza kuhusu mahali hapo, yaani ulimwengu halisi kabisa ambao tutauishi kwa kipindi cha miaka 1,000.
Tutafurahia wakati huo katika makao tunayoyaita yetu wenyewe, tukiwa na ardhi na mali ambazo haziwezi kamwe kunyang’anywa
Hatutakuwa na magonjwa na huzuni, kwa kuwa hakutakuwa na kitu chochote ndani yetu wala katika ulimwengu kitakachotatiza amani au furaha yetu.
Tutakuwa na kazi yenye maana ambayo si ngumu na na tutafurahia mahusiano mema pamoja na uzuri wa asili ambao Mungu ameuumba.
Na tutamjua, tutamwabudu na kumtumikia Bwana kwa njia ambazo hatuwezi hata kufikiria leo.
Hatuwezi kusema haswa jinsi dunia na bahari zinavyoonekana baada ya ukarabati, lakini jambo moja ni hakika
Ulimwengu wa Ufalme hautakuwa duni kwa kufurahia kuliko ulimwengu tunaoujua sasa.
Uzuri na ubora wa dunia ya Ufalme hautakuwa mdogo au chini ya uzuri na furaha inayopatikana katika duniani leo.
Kinyume chake, itakuwa kubwa zaidi
Na ingawa kuna mengi ambayo hatuwezi kujua kuhusu mahali hapo, bado kuna mengi tunayoweza kujua
Lengo letu katika somo hili ni kujifunza yale tunayoweza kwa muda mfupi ili ufahamu wetu kuhusu wakati huo ukue.
Na tunapoelewa zaidi kuhusu maisha yatakavyokuwa mahali hapo, tunaweza kuyatarajia zaidi
Na unapofikiria zaidi kuhusu maisha ya Ufalme, utaanza kuishi zaidi kwa ajili ya maisha hayo badala ya maisha haya.
Na kwa sababu kuna mengi tunayoweza kusema kuhusu Ufalme, tunahitaji kuikaribia sehemu hii ya somo letu katika sehemu au vipengele tofauti.
Kwanza, tutajifunza mabadiliko katika mpangilio wa uumbaji na katika maumbile, ikiwa ni pamoja na jiografia, mipaka na serikali ama utwala wa nchi.
Pili, tutajifunza kuhusu watu watakaokuwa katika Ufalme na ubora wa maisha ya kila siku katika wakati huo.
Tatu, tutajifunza nafasi ya Yesu katika Ufalme, pamoja na hali ya ibada katika Hekalu jipya la Ufalme.
Hatimaye, tunajifunza tukio la kilele la Ufalme: vita vya Gogu wa Magogu
Tuanzie na namna ambavyo uumbaji utabadilika wakati wa kipindi cha Ufalme, na somo hilo linaanza kwa kuangalia yaliyopita
Adamu na mwanamke walipotenda dhambi, Bwana alijibu dhambi yao kwa kutoa matamko kadhaa ya hukumu.
Bwana alijibu dhambi ya makusudi ya Adamu kwa kuilaani ardhi, yaani dunia yenyewe.
Mungu aliiweka dunia chini ya laana, na laana kutoka kwa Mungu ni tamko la hukumu linalosababisha uharibifu
Kwa hiyo, siku moja dunia itaharibiwa na kubadilishwa na nyingine, kama tutakavyoona hivi karibuni.
Wakati huo huo asili ya Uumbaji pia ilibadilika, kuanzia na hitaji la wanadamu kufanya kazi kwa bidii ili kuzalisha chakula kutoka ardhini.
Bwana alitangaza kwamba ardhi ingezaa miiba na michongoma kiasili.
Kwa hiyo, mbali na juhudi za mwanadamu, dunia ingezalisha magugu na mimea isiyo na manufaa.
Ni kwa jasho la uso wake tu ndipo mwanadamu angeweza kupata chakula anachohitaji.
Kabla ya laana, mwanadamu alifurahia maisha katika bustani iliyotoa chakula chote alichohitaji bila kazi yoyote.
Hakukuwa na magugu yaliyomea, wala mimea isiyofaa iliyozuia ukuaji wa mimea mizuri.
Adamu alihitaji tu kutoka nje ya makazi yake, na angepata chakula chote alichotaka.
Zaidi ya hayo, siku za mwanadamu zitahesabiwa, ikimaanisha kuwa maisha yatakuwa na mwisho unaoitwa kifo
Roho ya Adamu ilikufa mara tu alipokula tunda, na sasa mwili wake wa kimwili pia ungekufa.
Kila kitu kilichotoka ardhini kililaaniwa kama ilivyolaaniwa ardhi yenyewe, jambo lilomaanisha mwili wa mwanadamu ungekufa.
Vivyo hivyo, ufalme wa wanyama, ambao nao uliumbwa kutoka kwenye udongo, pia ungekufa
Bwana alianzisha mchakato wa kuoza ambao husababisha miili ya kimwili kushindwa na magonjwa na udhaifu kadri muda unavyoendelea
Kifo kinaweza pia kutokea kutokana na matendo ya ghafla ya vurugu, ambayo nayo ni matokeo ya dhambi.
Haya yote yalikuwa mabadiliko kutoka hali ya mwanzo, kwa sababu mwili halisi (au wa kimwili) uliumbwa kuishi milele.
Bila dhambi, Paulo anaelezea katika Warumi, kusingekuwa na kifo, kwetu sisi au kwa kiumbe kingine chochote.
Kwa hiyo, baada ya anguko la mwanadamu, mpangilio wa uumbaji ulibadilika kwa njia za msingi, ukijumuisha ugumu wa kufanya kazi ya ardhi na kifo cha mwili.
Kisha baadaye, baada ya gharika, Bwana alifanya mabadiliko mengine katika uumbaji, hasa katika ufalme wa wanyama.
Baada ya gharika, Bwana alimpa mwanadamu ruhusa ya kula nyama ya wanyama.
Kabla ya wakati huo, wanadamu walikula mimea tu kama Mungu alivyoagiza katika Bustani
Ingawa maandiko hayasemi wazi kwamba lishe ya wanyama ilibadilika, tunadhania kwamba baada ya wakati huo wanyama pia walianza kulana wao kwa wao.
Mabadiliko hayo yangekuwa ya lazima kwa sababu katika siku na majuma yaliyofuata baada ya gharika, mimea ingekuwa michache sana.
Kwa hiyo, kama kusingekuwa na nyama ya kula, wanyama wengi wangekufa kwa njaa.
Vile vile, mabadiliko katika hali ya hewa ya dunia kufuatia mafuriko yalifanya iwe vigumu zaidi kupanda mazao
Kisha ili kuwalinda wanyama kutokana na kutoweka haraka, Bwana aliweka uwanja wa michezo sawasawa (kwa maana ya kusawazisha hali ya maisha) kwa kuweka hofu ya mwanadamu ndani ya wanyama.
Hapo awali wanyama hawakuwa na hofu ya wanadamu wala ya wanyama wenzao, lakini sasa uhusiano wa mwindaji na mawindo yaani wanyama wanaowinda wanyama na mawindo ulianzishwa.
Wanyama wakawa maadui wao kwa wao, na pia kati ya wanadamu na wanyama kukawa na hali ya uadui.
Wanyama wangeweza kuwashambulia wanadamu, na wanadamu wangeweza kula wanyama.
Kwa hiyo ulimwengu tunaoujua leo ambapo watu na wanyama wanakulana, wanashambuliana, na hatimaye hufa unawakilisha mabadiliko ya kusudi la asili la Uumbaji.
Vivyo hivyo, ugumu tunaokutana nao katika kufanya kazi na mazingira ya asili ni mabadiliko kutoka kwenye mpango wa awali wa Mungu.
Mambo haya yalitokana na dhambi ya mwanadamu
Na katika siku zijazo Bwana ana mpango wa kurekebisha matokeo haya yote ya dhambi ya Adamu na anafanya hivyo kwa hatua.
Wakati wa Ufalme, ataanza mchakato wa marekebisho na ataukamilisha kikamilifu katika Mbingu Mpya na Dunia Mpya zitakazokuja baada ya kipindi cha Ufalme.
Moja ya mambo ya kwanza yenye kufariji tunayojifunza kuhusu utaratibu wa uumbaji katika Ufalme ni kwamba wanyama wataendelea kuwepo katika kipindi hicho pia.
Mara nyingi tunajiuliza: “Je, mnyama wangu kipenzi atakuwa pamoja nami mbinguni?”
Naam, mnyama wako kipenzi anaweza kuwa huko, lakini poodle wangu (mbwa wa kufugwa wa manyoya yaliyopinda) hatakuwepo…poodle huenda mahali pengine
Kila tunapojibu swali kuhusu mbinguni, ni lazima tuwe waangalifu na tueleze kwa usahihi ni mahali na wakati gani tunamaanisha.
“Mbinguni” si mahali au wakati mmoja tu… mbinguni ni pale Yesu alipo.
Na Yesu anazunguka-zunguka, na kwa hiyo sisi pia tunazunguka-zunguka pamoja naye.
Kwa upande wetu, mbingu huanza katika chumba cha enzi cha Mungu baada ya kifo au unyakuo.
Hiyo itakuwa nyumba yetu kwa muda mfupi, lakini si nyumba yetu ya kudumu, kwa sababu si mahali halisi pa kuishi.
Tumeumbwa kuishi katika dunia halisi, na ndivyo walivyo pia wanyama.
Lakini kwa kuwa wanyama hawana roho, hawatapatikana katika makao ya muda tuliyo nayo katika chumba cha kiti cha enzi cha Mbinguni.
Lakini Yesu atakapoturudisha duniani kwa ajili ya Ufalme, Isaya anasema tutawakuta wanyama duniani katika kipindi hicho.
Lakini kulingana na Isaya 11, asili ya ufalme wa wanyama itabadilishwa.
Wanyama wanaokula wengine kama mbwa mwitu, chui na simba wataishi kwa amani pamoja na mawindo kama kondoo, mbuzi na ndama
Zaidi ya hilo, wanyama wakubwa na hatari hawatakuwa tishio kwa wanadamu, na wanyama hawatakuwa na hofu ya mwanadamu.
Hata nyoka mwenye sumu (fira) hataleta hatari kwa mtoto mdogo, na kijana mdogo ataweza kuwaamuru wanyama watii.
Na kwa kuwa hawana sababu ya kuwaogopa wanadamu, wanyama hawa wataacha kuwashambulia wanadamu kwa njia za kujilinda zenye hatari zinazosababisha kifo.
Kwa kifupi, wanyama wote wataweza kufugwa katika siku hiyo, na watatii mapenzi ya mwanadamu, na tena tutakuwa na mamlaka juu ya ufalme wa wanyama.
Leo, wanyama wengi wa porini hawawezi kufugwa kwa sababu hawatabiriki na wanaweza kurudi kwenye tabia zao za porini.
Lakini katika siku hiyo, Bwana ataondoa uhusiano wa mwindaji na mawindo, hivyo hakutakuwa tena na wanaowinda wala wanaowindwa.
Huu ni ubadilishaji wa moja kwa moja wa tangazo ambalo Mungu alimpa Nuhu, na ni hatua ya kurudi kwenye asili ya awali ya ulimwengu.
Kisha, Bwana anabadilisha laana ya kufanya kazi ngumu ili kupata chakula katika maisha ya Ufalme
Akizungumzia kile ambacho Israeli watapitia katika Ufalme, Bwana anasema maisha yatakuwa rahisi
Bwana anaweka agano la amani na Israeli, na agano hilo linalirejesha tena taifa katika nchi yake
Na hapo ndipo Bwana atakapoifanya milima ya Israeli kuwa baraka tena
Anasema kwamba wanaweza kulala msituni salama bila hofu, jambo linaloashiria kwamba hawana adui, wa kibinadamu au wanyama.
Lakini basi, angalia kwamba miti ya mashambani itazaa matunda, na ardhi itatoa mazao mengi.
Haya ni maneno yanayorejelea uzalishaji wa asili wa ardhi bila hitaji la kulima au kuandaa mashamba.
Haya ni mabadiliko ya moja kwa moja ya laana juu ya dunia ambayo ilifanya maisha kuwa magumu na yenye taabu
Sasa laana hiyo imeondolewa, hivyo kufanya kazi shambani si kazi ngumu tena
Hili ni kweli kwa Israeli na kwa mataifa yote duniani
Kwa hiyo unaposikia kwamba tumepewa urithi katika nchi na maisha yetu yatakuwa ya kilimo, unahitaji kuelewa maana yake
Si maisha magumu na yenye taabu...bali ni kinyume chake
Kilimo ni furaha wakati ardhi inakupa mazao yake bila kuhitaji kuandaa ardhi au hata kupanda mbegu.
Bwana anasema nchi itakuwa kama Edeni tena na hakutakuwa na njaa tena katika nchi
Bwana ataita matunda na nafaka vitokee kwa ajili ya watu wake
Itakuwa vigumu kiasi gani kulima ardhi inayozalisha chakula kwa wito wa sauti ya Mungu?
Hii pia ni picha kubwa ya neema… Bwana ndiye anayefanya kazi, na sisi tunapokea baraka.
Mungu anawezaje kuhakikisha mafanikio makubwa ya kilimo katika jangwa?
Baada ya Bwana kuwaokoa Israeli, anawapa mambo mema aliyoyaahidi katika Ufalme
Kile ambacho hapo awali walikipitia kama upungufu na mateso katika wakati wa Dhiki, sasa watakuwa na kila kitu wanachohitaji.
Watapata mvua na malisho mazuri yenye nafasi kubwa kwa mifugo, pamoja na chakula cha kutosha.
Na Kisha tunasikia kwamba jiografia ya Israeli itakuwa tofauti sana na ilivyo leo.
Vijito vinatiririka kila mahali kwenye vilele vya milima, mvua ikinyesha popote wanapopanda mimea.
Jambo la kuvutia zaidi ni kwamba jua na mwezi vinaonekana kuongeza mwanga wake kwa kiwango kikubwa.
Haiko wazi kama Isaya anamaanisha haya kwa maana halisi au kama ni taswira ya lugha inayoonyesha mtazamo wa matumaini na furaha ya Israeli.
Yaani, katika siku hiyo, jua litaonekana kung’aa zaidi; lakini kama ni halisi, huleta maswali mengi kuliko majibu.
Tunawezaje kuishi kwenye sayari yenye mwanga mwingi kiasi hicho?
Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu ana njia ya kushughulikia mabadiliko haya na bado akatengeneza ulimwengu wenye uzuri na ustawi.
Na nina hakika kila mtu atakuwa na rangi ya ngozi yenye mvuto wa kupendeza.
Kwa hiyo Uumbaji katika Ufalme utakuwa karibu zaidi na hali ya wakati wa Edeni: huku wanyama wakimtii mwanadamu, hakuna wanyama wanaowinda na kuua wengine, na ardhi ikizalisha kwa urahisi.
Lakini jambo moja halitabadilika: laana juu ya Shetani na nyoka itaendelea katika kipindi chote cha Ufalme.
Huko nyuma katika Mwanzo 3, Bwana pia aliweka laana juu ya Shetani kwa jukumu lake katika anguko la mwanadamu.
Nyoka alikuwa kiumbe halisi aliyekaliwa na kutumiwa na Shetani, ambaye alimchukua nyoka huyo kama kificho ili kumdanganya mwanamke.
Kama matokeo ya wakati huo, Bwana alimlaani nyoka katika mstari wa 14
Nyoka alilazimishwa kutoa (au kupoteza) miguu yake na kutambaa ardhini
Hii inaonyesha kwamba kabla ya anguko, nyoka huenda alikuwa akitembea wima au angalau tumbo lake halikugusa ardhi.
Lakini tangu wakati huo na kuendelea, nyoka angekuwa karibu kabisa na ardhi, kama ukumbusho kwa wanadamu kuhusu mahali pao pa mwisho: udongo.
Ni wazi kwamba nyoka alikuwa mshiriki asiyejua wakati huo na hakupaswa kulaumiwa kwa matokeo.
Kwa hiyo laana ya Bwana dhidi ya nyoka haikukusudiwa kama adhabu dhidi ya mnyama
Badala yake, ilikuwa ukumbusho wa kuwakumbusha wanadamu wakati huo na adui yao wa kweli
Kwa hiyo kwa muda wote ambao Shetani atakapokuwapo na kwa muda wote ambao dhambi bado ni sehemu ya maisha duniani, nyoka angechukua umbo hili.
Kwa hiyo swali ni "je, laana hii itaondolewa katika kipindi cha Ufalme?" Jibu ni Hapana.
Katika Ufalme, Isaya anasema kwamba nyoka ataendelea kula mavumbi, jambo ambalo ni rejea ya moja kwa moja katika Mwanzo 3.
Kwa maneno mengine, umbo la nyoka aliyelaaniwa litaendelea bila kubadilika wakati wa Ufalme
Umbo lake halibadiliki kwa sababu hali zilizopelekea umbo hilo bado hazijabadilishwa kikamilifu.
Shetani bado yupo, ingawa amefungwa hadi mwisho wa Ufalme
Sasa, tuangalie mabadiliko mengine ya mipaka na jiografia yanayotokea wakati wa kufanywa upya kwa mbingu na dunia.
Kwanza, Israeli itakuwepo katika Ufalme, lakini mipaka ya Israeli itakuwa tofauti na ilivyo leo au wakati wowote uliopita.
Mungu ataweka mipaka mipya kwa Israeli, huku akiwaondoa maadui wa kihistoria wa Israeli waliowazunguka
Leo, Israeli inachukua eneo dogo sana kando ya Bahari ya Mediterania.
Lebanon iko upande wa kaskazini, Misri upande wa kusini, na Yordani na Syria upande wa mashariki.
Na eneo hili ni sehemu ndogo tu ya ardhi ambayo taifa hilo lilimiliki wakati wa kilele cha ufalme chini ya Sulemani.
Wakati huo, Israeli ilikuwa ufalme wenye nguvu zaidi duniani, nguvu kuu ya wakati huo.
Katika kilele chake, Israeli ilienea kufika kaskazini kabisa hadi Syria, ikijumuisha Lebanoni yote na ardhi yote iliyo mashariki mwa Yordani.
Na pia ilienea kusini hadi Misri na kusini mwa Yordani
Tangu wakati huo, Israeli haijawahi kudhibiti eneo kubwa kiasi hicho tena.
Tunaweza kutarajia kwamba Mungu angewapa Israeli ruzuku ya ardhi sawa na ardhi ile waliyoimiliki chini ya Daudi na Sulemani.
Lakini hiyo si hata nusu ya yote, kwa maana halisi.
Hebu turudi nyuma tuchunguze ahadi ya nchi ambayo Mungu aliahidi kwa Ibrahimu na uzao wake katika agano lake.
Mungu aliipa Israeli mipaka kuanzia mto wa Misri hadi mto Frati.
Mto wa Misri uko kwenye mpaka wa kihistoria wa Israeli huko Misri kwenye rasi ya Sinai
Na mto Frati uko Iraq, ambayo iko mbali sana mashariki kuliko mipaka yoyote ya kihistoria ya Israeli.
Baadaye Israeli walipoingia katika Nchi ya Ahadi chini ya Yoshua, Bwana alirudia kutaja mipaka ya nchi aliyokuwa akiwapa Israeli.
Bwana anafafanua kuhusu ugawaji wake wa ardhi akisema aliwapa Israeli nchi kuanzia jangwa hadi Lebanoni
Na kutoka mto mkubwa Frati hadi Bahari Kuu
Maelezo haya yanaenda mbali zaidi ya mipaka ya kitamaduni ya Israeli ya kihistoria.
Hii ndiyo mipaka ambayo Mungu ameahidi kuwa Iasraeli itakuwa nayo siku atakapotimiza ahadi zake kwa Ibrahimu, Isaka na Yakobo, na kwa Israeli.
Ezekieli anatupa viashiria vingine kadhaa katika Ezekieli 47:15-20, na tukivipanga viashiria hivyo vya kijiografia, tunafika kwenye Israeli tofauti kabisa
Israeli itamiliki eneo kubwa zaidi la ardhi kuliko lolote lilichowahi kuonekana hapo awali
Zaidi ya hilo, ahadi ya Mungu kwamba Israeli itatawala waliokuwa wakiwakandamiza inatimizwa kupitia mipaka hii.
Israeli itayameza mataifa yote yaliyowahi kuiudhi katika eneo hili kihistoria:
Moadi, Amoni, Edomu, Misri, Ashuru, Babeli na mengine kama Mungu alivyoahidi
Hivyo Israeli itakuwa kubwa zaidi kuliko ilivyowahi kuwa, na na itazimeza majirani zake.
Hatuna mipaka iliyotolewa kwa mataifa ya watu wa mataifa mengine, isipokuwa kwamba Biblia inataja kuwa mataifa mengi tunayoyafahamu yatakuwepo.
Muda hautoshi kuchunguza eneo hili kwa undani, na kama unataka ufahamu zaidi, unaweza kusikiliza somo la Ezekieli.
Lakini kwa muhtasari, mataifa mengi yatajazwa tena duniani kote na waamini wa Mataifa ingawa kuna tofauti chache.
Edomu itakuwepo katika Ufalme lakini itabaki tupu kama ukumbusho wa dhambi yao dhidi ya Israeli
Itakuwa mahali pa kuingilia shimoni ambapo Shetani atashikiliwa
Moshi utatoka katika shimo hio na hakuna mwanadamu atakayekanyaga katika nchi hii
Pili, Misri itakuwepo lakini Wamisri wa Ufalme hawataruhusiwa kuingia katika nchi yao kwa miaka 40 ya kwanza ya Ufalme.
Hii itakuwa kumbukumbu ya jinsi Misri ilivyoipotosha Israeli kwa ibada za sanamu, na kusababisha Israeli kutangatanga jangwani.
Lakini hatimaye, Misri itaruhusiwa kukaliwa baada ya miaka 40 kuisha
Hayo ndiyo mabadiliko makubwa ya kijiografia na mipaka ya Ufalme, lakini pia kuna mabadiliko ya asili katika ardhi katika Ufalme.
Mbali na ardhi kuwa na rutuba zaidi na mito mingi zaidi, kutakuwa na mabadiliko mengine makubwa ya kijiografia.
Kuanzia na mlima ambao Yerusalemu umejengwa juu yake.
Mlima huu utainuliwa juu sana na utawavuta watu kutoka kote ulimwenguni kuelekea huko
Mlima ulio katikati ya Israeli utakuwa mlima mrefu zaidi duniani
Juu ya mlima huu kutakuwepo hekalu, nyumba ya Bwana ambapo Kristo atakaa
Tutajifunza zaidi kuhusu hekalu katika somo lijalo
Kisha, Zekaria anasema kutakuwa na mito mipya inayotiririka kutoka juu ya mlima huu
Mji wa Yerusalemu utakuwa chanzo cha mito miwili, mmoja utakaotiririka upande wa Mashariki na mwingine upande wa Magharibi.
Mto unaotiririka magharibi utaishia katika Bahari ya Mediterania huku ule unaotiririka mashariki utaishia katika Bahari ya Chumvi.
Kulingana na Ezekieli, mto huu mpya unaotiririka mashariki utakuwa na athari kubwa kwenye Bahari ya Chumvi
Mto unaotiririka kutoka Mlima Sayuni utabadilisha Bahari ya Chumvi kuwa chanzo cha maji safi
Ezekieli hasemi ikiwa jambo hili litatokea kwa muujiza (ghafla) au kwa njia ya asili kwa muda, kama maji safi yanavyopunguza chumvi polepole.
Hata hivyo, muktadha wa andiko unaonyesha mabadiliko ya kimiujiza, hasa kwa kuzingatia kwamba ziwa hilo linajazwa na kila aina ya samaki.
Kwa hiyo, Bahari ya Chumvi inafufuliwa na kuwa picha nzuri ya kipindi cha Milenia ya neema ya Mungu kuleta uzima mahali palipokuwa na mauti.
Ezekieli anaongeza kwamba kutakuwa na wavuvi watakaovua huko, kutoka Engedi kusini karibu na Masada hadi Eneglaimu, ambayo haijulikani wazi lakini huenda iko mahali fulani kaskazini.
Watavua kulingana na aina zao, ikimaanisha kutakuwa na aina nyingi sana za samaki kiasi kwamba wavuvi watakuwa na utaalamu maalum wa kuvua kila aina.
Na samaki watakuwa wengi mno
Hata hivyo, maeneo ya chumvi yatabaki, pengine kama ushuhuda wa jinsi Bwana alivyobadilisha maji kutoka chumvi kuwa safi.
Zekaria 14 inatupa maelezo machache ya ziada ya kuvutia kuhusu nchi
Majira yataendelea kama yalivyo leo, kwa hiyo maisha yataendelea kuwa na mdundo kama tunaoufahamu leo
Na Zekaria anasema nchi inayozunguka Yerusalemu itabadilishwa kuwa uwanda mkubwa tambarare unaoenea kwa maili nyingi
Tutaendelea kujifunza zaidi kuhusu matumizi ya uwanda huu katika somo la baadaye.
Hatimaye, juu ya kilele cha mlima kutakuwa na hekalu na kiti cha serikali ya kipindi chote cha Ufalme.
Mataifa ya dunia, popote yatakapokuwa, yataelekea Yerusalemu kujifunza kutoka kwa Mungu wa Israeli
Na sheria za ulimwengu zitatoka Sayuni, kutoka katika neno la Bwana
Kwa hiyo mji mkuu wa Dunia utakuwa Yerusalemu, ambapo Bwana anakaa akitawala mataifa.
Tutajifunza zaidi kuhusu makao ya Bwana katika somo lijalo
Na katika mst. 3, Mika anasema Bwana ataamua kati ya mataifa ikiwa ni pamoja na mataifa yenye nguvu yaliyo mbali
Kutawala watu kunamaanisha kwamba wanahitaji utawala ili kufanya mambo sahihi
Hiyo ni ishara kwamba dhambi ipo, na kwa hiyo ulimwengu unahitaji hukumu kamilifu ya Kristo ili kuhakikisha mwenendo sahihi
Lakini Kristo anatawala kwa ukamilifu kiasi kwamba anaweza kudhibiti dhambi hata upande mwingine wa dunia.
Kristo hutekeleza utawala wake mkamilifu kupitia serikali inayofanya mapenzi yake kikamilifu
Isaya anasema kwamba, maafisa wa serikali yake watajua mapenzi yake mara moja ili kuyatekeleza daima
Serikali yake itahakikisha kwamba hakuna dhambi itayopata nafasi ya kukua au kuondoa amani duniani
Kwa hakika, Mika anasema kwamba zana za vita zitaondolewa na sanaa ya vita itasahaulika kabisa.
Kwa hiyo ingawa dhambi itakuwepo, lakini haitakuwa na athari yoyote ya kimwili kwenye maisha kwani itakuwa chini ya utawala mkamilifu wakati wote.
Mtunga Zaburi anaelezea utawala wa Bwana kwa njia hii:
"Bwana atawaponda (au atawatawala) kwa fimbo ya chuma.
Anavunja upinzani wa mataifa yenye dhambi kama vyombo vya udongo vinavyosambaratishwa.
Lakini pia angalia kwamba kuna wafalme na waamuzi wa dunia katika siku hiyo, ambao Mika anasema wanapaswa kuonyesha uamuzi wa hekima katika kutawala.
Kwa hiyo, hii ina maana kwamba kutakuwa na serikali chini ya Yesu, serikali itakayotawala pamoja na Yesu chini ya mamlaka Yake.
Serikali hiyo itatekeleza maagizo Yake kikamilifu ili kuhakikisha kwamba dhambi inatawaliwa kwa ukamilifu.
Serikali iko juu ya mabega Yake, ikimaanisha Yesu ndiye anayesimamia utawala wenye mfumo wa kiutawala.
Dunia ni kubwa, na kutakuwa na wengi wa kutawala, kwa hiyo Kristo atawashirikisha wengine katika serikali Yake, ikiwa ni pamoja na sisi.
Na serikali hiyo imegawanywa katika serikali ya Kiyahudi na serikali ya Mataifa
Israeli, taifa ambalo hapo awali lilitawaliwa na wengine kwa nyakati nyingi, sasa litatawala dunia nzima
Na mfalme wao mashuhuri zaidi atarudi kuwatawala kama mkuu wao, akihudumu chini ya mamlaka ya Mfalme, Yesu.
Daudi atafufuliwa na kurudi kutawala nchi ya Israeli katika serikali ya Kristo.
Anaitwa mkuu kwa sababu Yesu ni Mfalme
Chini ya Daudi, makabila kumi na mawili ya Israeli yatatawaliwa na mitume kumi na wawili, kama Yesu alivyoahidi.
Mitume kumi na wawili watatawala makabila ya Israeli kama Yesu alivyoahidi
Makabila ya Israeli yatakuwepo katika nchi yao na yatakuwa na watawala wengine wa ziada juu yao.
Tunaweza kudhani kwamba watawala hawa wa ziada watakuwa watakatifu wengine wakubwa wa Agano la Kale waliopewa nafasi za heshima kama thawabu kwa huduma na uaminifu wao.
Tukielekea kwa mataifa mengine (Mataifa), tunapata maelezo machache zaidi, ingawa bado tunaweza kujifunza mambo kadhaa.
Kwanza, mataifa ya watu wa Mataifa yatakuwa yamesambaa duniani kote, na hivyo nayo yatakuwa na haja ya uwakilishi wa kiutawala.
Na wewe na mimi tutatimiza hitaji hilo: watakatifu wa kanisa watawatawala
Tayari tumeona hili katika Ufunuo 20, tuliposikia kwamba watakatifu wa kanisa watatawala pamoja na Kristo.
Pia Yesu alifundisha mifano akisisitiza kwamba atawalipa wale walio waaminifu hapa na sasa kwa kuwapa nafasi ya kuwa waaminifu katika mambo makubwa zaidi.
Katika mfano wa watumishi waliopewa fedha katika Luka 19, Yesu aliwapa watu waliokomaa kiroho nafasi ya kutawala miji.
Mfano huo unaonyesha jinsi Kristo atakavyotupatia majukumu katika serikali ya Ufalme
Unaweza kusema kwamba hujali kama utakuwa na cheo cha juu katika serikali ya Ufalme, lakini Yesu analitoa jambo hilo kama thawabu inayotamaniwa.
Kwa hiyo tunapaswa kutamani kumpendeza Yeye sasa na pia katika Ufalme ujao, Paulo anasema katika 2 Wakorintho 5
Hatimaye, tunahitaji kuelewa kwamba mataifa yote hayatafanana kwa hadhi katika enzi hii.
Israeli itakuwa taifa la juu zaidi duniani na mataifa mengine yote yataitumikia Israeli
Mataifa (wasiokuwa Wayahudi) yatatumikia Israeli, na Bwana ataiinua Israeli juu ya mataifa mengine yote kwa heshima na hadhi.
Hili ni badiliko kamili la nafasi ambayo Israeli imekuwa nayo kihistoria tangu wakati Bwana alipoanza kuliadhibu taifa hilo kwa sababu ya dhambi zake.
Sasa wanapokea baraka zao chini ya ahadi za Mungu
Inafaa kukumbuka jinsi Israeli ilivyofikia hatua hii ya utukufu
Waliumbwa kama taifa na Mungu kupitia Ibrahimu, wakapokea ahadi
Waliingia katika agano la kitaifa ili kupata baraka za Mungu
Walivunja Agano la Kale na hivyo walitumia miaka mingi kama watu walio chini ya hukumu ya Mungu
Walitawanywa kati ya mataifa na wakapata hasara kubwa.
Hatimaye walipitia na kustahimili kipindi cha Dhiki Kuu, ambapo Mungu aliwaleta kwenye mwisho wa nguvu na uwezo wao wenyewe.
Mwishoni, walimwamini Masihi wao na kumpokea.
Yeye atawaokoa na kuwaletea baraka zilizoahidiwa katika agano, na kuwafanya watii sheria ya Mungu kikamilifu.
Naye atawafanya kuwa taifa kuu duniani
Sasa, hitaji hili lote la serikali na utawala linaonyesha kwamba kutakuwa na kutotii katika kipindi hicho.
Na kutotii kunamaanisha dhambi, na hivyo maswali yanakuja: dhambi itakuwaje na kwa nini itaendelea kuwepo katika Ufalme?
Na tutajibu swali hilo wiki ijayo