Taught by
Stephen Armstrong
Taught by
Stephen ArmstrongMwisho wa Ufalme umefika, na bado kuna mambo ambayo hayajakamilika.
Tumejifunza mambo muhimu ya miaka elfu moja ya utawala wa Kristo duniani
Tulijifunza kuhusu maisha ya ajabu yaliyoandaliwa kwa ajili yetu sote katika mahali hapo, ambayo yatajiri hivi karibuni duniani.
Na tulijifunza kwamba baada ya kipindi hiki kuisha, kutakuwa na vita vya mwisho vya kuhitimisha Uumbaji
Vita hivyo vinatimiza kusudi la Mungu kwa ajili ya utawala wa Kristo, na kama Paulo alivyoeleza katika 1 Wakorintho 15, maadui wote wa Kristo hatimaye wataangamizwa.
Kisha tunapata uzoefu wa miaka 7+ ya usafi kabla ya uumbaji huu kuondolewa kabisa.
Muda huo wa ziada ulioongezwa mwishoni mwa Ufalme utakuwa ushuhuda wa uaminifu wa Mungu kwa Israeli.
Na miaka hiyo saba itakuwa kipindi cha pekee, chenye matukio yake ya kipekee kabisa.
Itakuwa wakati wa kipekee ambapo wanadamu wote wataokolewa na kuamini na hakutakuwa na adui wa Mungu akifanya kazi duniani.
Miaka hiyo saba itakuwa karibu zaidi na maisha ya Bustani ya Edeni kuliko wakati mwingine wowote, kama mwanamume na mwanamke walivyokuwa wakiishi.
Na sasa kilichobaki ni hukumu kuu kwa wote waliompinga Mungu katika enzi (historia) yote ya Uumbaji na Ufalme
Hapo ndipo tunapoanzia usiku wa leo…tukianzia na Shetani mwenyewe
Baada ya miaka 1,000 kumalizika na vita kuisha, Shetani atahukumiwa.
Lakini angalia kwamba hukumu yake si mwisho wa kuwepo kwake, bali ni mwanzo wa kuwepo katika hali mpya ya adhabu ya mateso.
Shetani anaungana na nabii wa uongo na Mpinga-Kristo katika Ziwa la Moto.
Nabii wa uongo na Mpinga Kristo waliingia katika Ziwa la Moto mwanzoni mwa Ufalme
Wakati huo, nilisema tutasubiri kulichunguza eneo hilo hadi tutakapofika mwisho wa Ufalme.
Kwa hiyo leo tunajifunza kile tunachoweza kuhusu mahali pa mwisho pa hukumu na jinsi adui pamoja na wanadamu wasiomcha Mungu watakavyoingia humo.
Tunaanza kwa ukweli kwamba mahali hapo kweli papo na panaendelea kuwepo milele
Kwa kweli, mahali hapo tayari papo sasa, lakini pako wapi? Katika Ufunuo 14 tulijifunza hivi:
Inaonekana kwamba ziwa hilo lipo katika maeneo ya mbinguni yaliyo nje ya uwezo wetu wa kuona, na lipo “mbele ya malaika.”
Kwa sasa ni tupu, na katika kipindi cha Ufalme wa miaka 1,000 litakuwa na Nabii wa Uongo na Mpinga-Kristo pekee.
Lakini mara baada ya vita vya Gogu na Magogu, Shetani ataungana nao, akiwaunganisha tena washiriki wote watatu wa Utatu wa Uongo
Mahali hapa ni makao ya wasiomcha Mungu na wasioamini milele yote
Angalia katika Ufunuo 20:10 kwamba Shetani atateswa humo milele na milele.
Hii ni kauli iliyo wazi kabisa, isiyo na utata na inathibitishwa pia na mistari mingine mingi katika Agano la Kale na Agano Jipya.
Katika Mathayo 25:46 , Yesu anathibitisha kwamba hukumu ya kutoamini inahusisha adhabu ya mateso ya kimwili milele na milele bila nafuu.
Tunaposikia haya, tunajiuliza kwa kawaida kuhusu haki ya mpangilio kama huo
Tunaweza kudhani kwamba adhabu hiyo haiendani na kosa hilo, kana kwamba Ziwa la Moto ni gereza ambapo wasiomcha Mungu hulipa deni lao mbele za Mungu.
Kwa mtazamo huo, tungetarajia kwamba baada ya muda fulani wangekuwa tayari wamelipa deni hilo.
Lakini hiyo si njia sahihi ya kuelewa adhabu ya milele
Sio mahali pa kufidia au kusamehe…ni mahali pa kukaa kwa wale ambao hawawezi kuingia mbele za Mungu.
Hiyo ndiyo maana ya kifo cha kiroho: ni kutengwa milele na uwepo wa Mungu.
Kama vile mustakabali wa mwamini ulivyo uzima wa "milele", ndivyo mustakabali wa asiyeamini ulivyo wa milele pia.
Biblia pia huita hii Mauti ya Pili, ambayo hufafanuliwa kama kukaa milele mbali na Mungu
Mauti ya Pili ni ya milele kwa sababu uovu, asili ya kuanguka ya Shetani, mapepo yake, na wanadamu wote wasioamini hudumu milele
Baada ya kifo hakuna nafasi ya pili ya wokovu, hivyo wote hubaki katika mateso mbali na uwepo wa Mungu milele.
Hawalipi deni lao kama katika gereza; bali wanaishi katika hali ya maisha yanayofaa kwa asili yao ya dhambi inayoendelea
Kwa hiyo baada ya Ufalme na Vita vya Gogu, kutakuwa na viumbe watatu katika Ziwa la Moto, na bila shaka wote wanastahili kuwa hapo.
Lakini Bwana aliwatupa huko bila utaratibu rasmi au kuendesha kesi ya hadhara na ni wazi kwamba hukumu zake zikichunguzwa, huonekana kuwa za haki.
Hukumu zake ni za haki siku zote na hakuna mtu anayesimama kumhukumu Mungu
Hata hivyo, Bwana atawapa wanadamu wengine aina ya kesi ya hadharani kabla ya kukabiliwa na hukumu yao.
Na katika maandalizi ya tukio hilo, wafu wasioamini watafufuliwa katika miili mipya kama sisi tulivyofufuliwa hapo awali.
Kumbuka kwamba Ufufuo wa Kwanza ulikuwa kwa ajili ya waamini wote, ilhali Ufufuo wa Pili ni kwa ajili ya wasioamini wote.
“Hao wafu waliosalia” wanaotajwa katika mstari wa 5 ni wale wote ambao hawakufufuliwa katika Ufufuo wa Kwanza kabla ya kuanza kwa Ufalme.
Huu ni ufufuo wa pili, na si tukio la baraka
Hapo ndipo tulipo sasa—katika wakati ambapo Ufalme umekwisha, wasioamini wote wamekwisha kufa, na wakati umefika wa kuhitimisha mambo yote.
Kama vile Ufalme usingeweza kuanza hadi waamini wote kutoka kizazi hiki walipokuwa tayari kuuingia pamoja...
vivyo hivyo hukumu ya mwisho isingeweza kufanyika hadi wasioamini wote walipokuwa tayari kuhukumiwa.
Na sasa mwishoni mwa Ufalme, wasioamini wote wako tayari kukabiliana na hukumu
Yohana anaona kiti cha enzi kikubwa cheupe kikitokea na mtu asiyetajwa jina ameketi juu yake, lakini tunajua huyu ni Yesu
Yohana na Petro wanatuambia kwamba Yesu ameteuliwa na Baba kuhukumu (ama kuwa mwamuzi) wa watu wote
Hapo awali Yesu aliwahukumu walio hai, yaani waaminio, alipotupatia thawabu zetu za milele katika Kiti cha Hukumu cha Kristo.
Na sasa Yesu ameketi kwenye Kiti Kikuu Cheupe cha Hukumu akiwa tayari kuwahukumu wafu, ikimaanisha wasioamini
Na hukumu hii inapoanza, Yohana anasema Dunia na Mbingu zitakimbia
Neno "mbingu" katika muktadha huu linarejelea mbingu ya kwanza na ya pili, uumbaji halisi
Kwa hiyo hukumu hii inapoanza, ulimwengu wote unatoweka kwa muda mfupi
Neno la Kigiriki la "zikakimbia" ni pheugo , ambalo linamaanisha kukimbia
Ni neno lile lile ambalo Mtume Marko anatumia kujielezea akikimbia uchi baada ya kukamatwa bustanini
Hebu fikiria jinsi Marko alivyokimbia kwa kasi akiwa uchi ili kujificha. Huo ndio mfano unaotupa picha ya jinsi uumbaji huu wa sasa utakavyotoweka kwa ghafla.
Kisha wanadamu wote wa nyakati zote watakuwa wamekusanyika mbele ya kiti cha enzi katika wakati huo.
Hebu fikiria ni roho ngapi hizo zitakuwepo? Wote ambao wamewahi kuishi kwenye sayari ya dunia kwa takribani miaka elfu saba
Ni Mabilioni kwa mabilioni ya watu watakuwapo hapo. Ni vigumu hata kuwaza idadi hiyo, lakini wewe pia utakuwepo.
Hata hivyo, tutakuwepo katika hali ambayo hakuna uumbaji wa kutushikilia, jambo ambalo pia haliwezi kufikirika.
Mwanga pekee utakuwa Yesu Mwenyewe, kwa kuwa jua litatoweka, na hakutakuwa na dunia chini ya miguu yetu.
Kwa hiyo wasioamini wote wanafufuliwa na kusimama mbele ya Kristo katika wakati huu, wakubwa kwa wadogo (ni hukumu inayowahusu wote bila upendeleo.)
Wanahukumiwa kutokana na vitabu vilivyopo wakati huo, lakini kwanza wafu wote wanatoka wapi? Wamekuwa wapi kwa muda wote huu?
Kwanza, hebu tupitie kinachotokea mtu anapokufa, kwa sababu matokeo hutofautiana kulingana na mtu ni nani na amekufa katika kipindi gani cha historia.
Wanadamu wana roho (au nafsi) na mwili, na roho yetu ni ya milele huku miili yetu ikiwa ya muda mfupi.
Miili yetu huharibika kila wakati roho yetu inapoondoka, lakini roho yetu huendelea kuishi katika moja kati ya hali mbili.
Kwa watakatifu, mahali pa roho zao ni mahali pa faraja, na mahali hapo hutegemea kipindi cha historia ambacho mtu alikufa, kulingana na Maandiko.
Kabla ya Kristo kuja, waamini walienda Kifuani mwa Ibrahimu wakingojea kuwasili kwa Masihi.
Baada ya Kristo kufa na kuwaweka huru mateka hawa, roho ya mwamini ilienda moja kwa moja Mbinguni ili kuwa pamoja na Yesu milele.
Katika Ufufuo wa Kwanza, waamini kutoka nyakati zote hupokea miili mipya na tangu wakati huo hubaki pamoja na Yesu milele.
Lakini kwa wasioamini, mahali pa roho zao daima pamekuwa pale pale: mahali pa mateso panapoitwa Hadesi (au Kuzimu), na baadaye Ziwa la Moto.
Na katika mstari wa 13 tunaambiwa mahali ambako wafu hawa watatokea katika ufufuo wao.
Kwanza, Hadesi (Kuzimu) itawatoa wafu wake. Hii ni rejea ya wasioamini wote kuondolewa kutoka mahali hapo.
Kila mtu asiyeamini tangu siku za Kaini atakuwa akiishi Hadesi kwa wakati huu isipokuwa wanadamu wawili.
Mpinga-Kristo na Nabii wa Uongo hawatakuwapo tena Hadesi, kwa sababu tayari watakuwa wametupwa katika Ziwa la Moto.
Wengine wote sasa wataondolewa kutoka mahali hapo baada ya kukaa humo kwa mamia na maelfu ya miaka wakisubiri siku hii.
Pili, bahari itawatoa wafu wake, na rejea ya bahari inaweza kuonekana ya kutatanisha, kwa sababu hapa imetumiwa kwa njia ya tashbihi (yaani kwa maana ya mfano).
Ni rejea ya shimo lisilo na mwisho (Abyss), mahali pa kufungwa kwa mapepo, lililo karibu na Hadesi katikati ya dunia.
Katika Biblia bahari ni picha au taswira ya kuzimu, mahali pa kufungiwa malaika wasiomcha Mungu.
Kwa Kiebrania neno tehom linaweza kutafsiriwa kama shimo (kama vile shimoni) au kama bahari
Na hilo linaonyesha jinsi Wayahudi walivyoelewa bahari kuwa sitiari (au mfano au picha) ya shimo la kuzimu na ndivyo Yohana anavyoitumia hapa
Hukumu hii ni kwa ajili ya wanadamu wasiomcha Mungu na malaika wasiotii pia, kwa hiyo wanafufuliwa kutoka gerezani mwao ili wahukumiwe pia.
Mapepo yanaujua wakati huu na yamekuwa yakiusubiri kwa hofu, yakijua kwamba siku hiyo lazima itafika.
Hatimaye, Yohana anasema kwamba “mauti” inawatoa wafu waliokuwa chini yake. Hapa anarejelea kifo cha kwanza, ambacho kimekuwa hali ya wanadamu (yaani kikifanya kazi) hadi wakati huo.
Tazama kwamba “mauti na Kuzimu (Hadesi)” vinatajwa pamoja, na vinatofautishwa na “bahari”, ambayo mara nyingi hueleweka kuwa ni shimo lisilo na mwisho (abyss).
Shimo hilo limeandaliwa kwa ajili ya mapepo, ilhali mauti na Hadesi vinawahusu wanadamu, kwa kuwa sisi tuna miili inayokufa.
Kwa hiyo Kifo cha Kwanza kinawatoa wafu wake kwa maana kwamba kinafikia mwisho wake
Hivyo basi, kifo si mahali, bali ni hali ya kuwepo....Kwa maana hiyo, "kifo" kinawaachilia wale ambao walikuwa chini ya nguvu zake.
Na badala yake itakuja Mauti ya Pili
Na kwa kuwa kifo chenyewe pamoja na dunia ya sasa vinapita, basi Hadesi nayo haitakuwepo tena.
Kwa hiyo wanadamu wote wasioamini sasa watasimama pamoja, waasi wanaompinga Mungu na tunaweza kudhani kwa usalama kwamba huu lazima uwe wakati wa huzuni kubwa na wa kutisha sana.
Dhambi zote ambazo hazikutubiwa za ulimwengu zitafunuliwa wazi kwa wakati mmoja.
Sisi pia tulizaliwa katika hali ileile kama wao, na kama isingekuwa kwa neema ya Mungu, nasi tungesimama mahali hapo.
Daima kumbuka kwamba umeokolewa usiupitie wakati huo, si kwa sababu ya sifa au ustahili wako, bali kwa sababu ya rehema ya Mungu pekee.
Lakini wakati huu, kila goti litapigwa na ulimi utakiri kwamba Yesu ni Bwana
Ndimi zao zote zinamkiri Yesu kuwa ni Bwana, lakini wakati huu kukiri huko hakuwaletii wokovu, kwa sababu wanakiri jambo lililo dhahiri.
Kukiri kwao hakufanywi kwa imani katika Neno la Mungu.
Badala yake, ni kukiri ukweli ulio wazi kabisa; na kwa kuwa hakuhitaji imani, hakuna wokovu unaopatikana kupitia kukiri huko.
Kisha katika mstari wa 12 roho hizi zinahukumiwa kulingana na vitabu vilivyofunguliwa mbele yao na pengine yaliyomo katika vitabu hivyo yanasomwa hadharani kwa sauti.
Tazama kwamba kuna aina mbili za vitabu vinavyotajwa: Kitabu cha Uzima na vitabu vya matendo.
Kitabu cha uzima kimetajwa katika sehemu mbalimbali katika Maandiko Matakatifu
Kutokana na vifungu hivi vya Maandiko, tunajifunza kwamba Kitabu cha Uzima ndicho ambamo Bwana ameandika majina ya wote waliopokea rehema zake.
Ni kumbukumbu ya familia ya wana na binti za Mungu, na majina hayo yaliandikwa katika kitabu hicho kabla ya kuumbwa kwa ulimwengu.
Hii inaonyesha kwamba hata kabla ya Adamu na mwanamke kuumbwa, Bwana tayari alikuwa amekusudia kuwa na familia yake mwenyewe.
Na historia yote ya wanadamu imeendelea kulingana na mpango wa Mungu hadi kila jina lililoandikwa katika Kitabu cha Uzima lilipozaliwa duniani.
Baada ya kuzaliwa, watu hao waliokolewa kwa njia ya imani, na baadaye walifufuliwa katika ufufuo wa kwanza.
Kwa hiyo basi, ikiwa hukumu ya Kiti Kikuu Cheupe cha Enzi ni kwa ajili ya wasioamini pekee, kwa nini Kitabu cha Uzima kipo hapo?
Jibu ni rahisi: uwepo wake unathibitisha kwamba hakuna hata mmoja wa wale waliosimama mbele ya hukumu hiyo anayestahili kuhesabiwa kuwa hana hatia au kupewa uzima wa milele.
Hakuna hata mmoja wao aliyemkiri Kristo, hakuna aliyepokea msamaha, hakuna hata mmoja aliye katika familia ya Mungu.
Huenda huu ndio wakati unaokaribia zaidi katika Biblia na simulizi (hadithi) ya zamani maarufu ya kubuni kuhusu Petro anayesimama kwenye Milango ya Lulu akihakiki majina katika orodha.
Kwa kuwa hakuna hata mmoja atakayepatikana ameandikwa katika Kitabu cha Uzima, kinachobaki ni kuhukumiwa kwa msingi wa vitabu vingine vilivyopo kwenye hukumu hiyo.
Yohana anasema kwamba wafu watahukumiwa kutokana na mambo yaliyoandikwa katika vitabu hivyo, kulingana na matendo yao.
Sasa, vitabu hivyo ni nini hasa? Kuna majibu mawili ambayo yamependekezwa
Jibu la kwanza ni kwamba vitabu hivyo vina kumbukumbu ya kila tendo la dhambi ambalo kila mtu amelifanya, na matendo hayo ndiyo yanayowafanya wastahili hukumu.
Maisha ya kila mtu ni hadithi ndefu ya dhambi, na bila neema ya Mungu iliyodhihirishwa katika Yesu Kristo, matendo yetu wenyewe yanatuhukumu.
Hapo ndipo swali linazuka: tukio hili litadumu kwa muda gani?
Itachukua muda gani kuwahukumu mabilioni ya watu ikiwa kila tendo baya la maisha ya kila mmoja litasomwa hadharani?
Uwezekano wa pili ni kwamba vitabu vinavyofunguliwa ni vitabu vitano vya Musa, yaani Sheria kwa maneno mengine
Ikiwa ndivyo ilivyo, kusomwa kwa vitabu hivyo kungekuwa kwa kusudi la kuorodhesha au kutangaza viwango vya haki ambavyo Mungu anavitaka.
Kisha kila mtu angehukumiwa kwa kuangaliwa kama ametimiza au ameshindwa kutimiza matakwa ya Sheria.
Katika hali hiyo, hukumu ingekuwa fupi zaidi, kwa sababu ingehitaji kutajwa dhambi moja tu katika kesi ya kila mtu.
Kwa maana mtu avunjapo amri moja tu, huwa mvunjaji wa Sheria yote, na hivyo anastahili hukumu
Angalia Yohana anasema katika mstari wa 15 "ikiwa" mtu yeyote hakupatikana ameandikwa katika Kitabu cha Uzima, basi atahukumiwa. Kauli hiyo inaweza kuonekana kana kwamba huenda baadhi yao wakapatikana.
Lakini ukweli ni kwamba hakuna hata mmoja atakayepatikana. Utafutaji huo haukusudiwi kuwathibitisha (kuwatetea) kuwa hawana hatia, bali kuthibitisha hukumu yao.
Kama mtu yeyote angeandikwa katika kitabu cha uzima, asingekuwa amesimama mahali hapo wakati huu.
Wangekuwa tayari wamejumuishwa katika ufufuo wa kwanza
Kwa hiyo, kwa kuwa wote watashindwa kipimo hicho, wote watatupwa wakiwa hai katika Ziwa la Moto, kama Yohana anavyosema.
Wanatupwa "wakiwa hai" kwa maana kwamba wanaendelea kuwa na fahamu na kutambua kikamilifu hali yao.
Huu ni uthibitisho tena kwamba Kifo cha Pili si maangamizi ya kutoweka kabisa bali ni uhai mpya wa milele yaani kuingia katika hali ya milele ya adhabu yenye ufahamu.
Kwa wakati huo, ulimwengu huu wa sasa—ambao umekuwa makao ya wanadamu kwa takribani miaka 7,000—utakuwa umepita, pamoja na wote waliompinga Mungu.
Watakaobaki ni watakatifu walio katika miili ya utukufu wa milele, malaika, na Utatu wa Mungu.
Na hilo linatuleta kwenye enzi inayofuata ya umilele, wakati wa siri kubwa katika Maandiko
Yote tunayojua kuhusu kile kinachofuata Ufalme yametolewa katika sura mbili tu za Biblia, sura mbili za mwisho
Ufunuo 21 na 22 zinatuambia kuhusu Mbingu Mpya na Nchi Mpya ambazo zitachukua nafasi ya zile tulizonazo sasa.
Hata hivyo, sura hizo zinaibua maswali mengi kuliko zinavyotoa majibu. Hilo linaendana na mtindo wa Mungu wa kujifunua hatua kwa hatu (huu ni muundo wa kibiblia wa ufunuo unaoendelea).
Katika historia yote, Mungu amekuwa akijifunua kwa wanadamu kwa namna ya ufunuo unaoongezeka taratibu.
Tunauona mtindo huo tunaposoma Agano la Kale na Agano Jipya, ambapo manabii waliendelea kupewa ufahamu zaidi kadiri wakati ulivyopita.
Mtindo huu unaonekana kuendelea hata kuhusu Mbingu Mpya na Dunia Mpya, kwa sababu kwa sasa Bwana ametufunulia sehemu ndogo tu ya yale yatakayokuja.
Labda tutakapokuwa katika Ufalme, Bwana atatupa uelewa zaidi wa kile kitakachofuata baada yake.
Kwa hiyo, kuhusu Mbingu Mpya na Nchi Mpya, tunaweza kusema kwamba sisi ni kama watakatifu wa Agano la Kale—tunajua sehemu ndogo tu kwa sasa, tukingoja ufunuo kamili katika wakati ambao Mungu ameukusudia.
Tunapojifunza sura mbili za mwisho za Biblia, tutakuwa pia tukirejea mara kwa mara sura mbili za kwanza za Biblia, kwa sababu moja imeundwa kwa mtindo unaoakisi nyingine.
Angalia mara moja jinsi Ufunuo sura ya 21 inavyoanza kwa kusema kuwa Mbingu Mpya na Nchi Mpya zimeumbwa.
Linganisha hilo na Mwanzo 1:1
Usambamba huu utaendelea hadi sura ya 22, na kila tutakapoukutana nao, tutauonyesha na kueleza kusudi lake.
Tofauti na Mwanzo sura ya 1, hatupewi maelezo ya kina kuhusu jinsi Nchi Mpya itakavyokuwa, isipokuwa maelezo machache yanayochochea shauku ya kujua zaidi.
Jambo la kwanza tunaloambiwa katika mstari wa 1 ni kwamba ulimwengu huu mpya hautakuwa na bahari hata moja.
Hili ni tofauti kabisa na dunia ya sasa, ambayo sehemu yake kubwa imefunikwa na bahari kuliko nchi kavu.
Kwa nini Mungu aliweka bahari katika uumbaji wa kwanza, lakini hakuzijumuisha katika uumbaji mpya?
Maandiko yanatufundisha kwamba Mungu hafanyi makosa wala habadili mawazo yake. Kwa hiyo, hatuwezi kusema kwamba aliboresha tu muundo (mpango) wake wa kwanza.
Lazima kuwe na sababu iliyofanya bahari ziwe nzuri na zifae katika uumbaji wa kwanza, lakini zisiwe na ulazima katika uumbaji mpya.
Kwa kuwa jambo hili litajitokeza tena katika sura hizi, tutangoja hadi tupate maelezo yote ndipo tutakapojaribu kufumbua fumbo hilo.
Kisha, Bwana anaweka mji katika dunia hii mpya, unaoitwa Yerusalemu Mpya lakini mji huo haujajengwa na wanadamu katika dunia mpya.
Badala yake, Bwana mwenyewe anauleta mji huo kutoka mbinguni na kuushusha duniani.
Maandiko yanatufundisha kwamba mji huu tayari upo sasa hivi katika ulimwengu wa mbinguni ukingoja siku hii ijayo ambapo utafunuliwa na kushushwa duniani.
Kushuka kwa Yerusalemu Mpya kutashuhudiwa kutoka duniani, na mwonekano wake utakuwa kama wa bibi-arusi aliyekwisha kujitayarisha kwa ajili ya mume wake.
Hebu fikiria wakati unapogeuka kutazama chini kwenye njia ya harusi ili kumtazama bibi harusi akitokea na kuelekea kwa kwa utulivu kwa bwana harusi wake.
Ni wakati wa kusisimua, unaotarajiwa kwa hamu na unaosherehekewa kwa furaha. Ndivyo itakavyokuwa wakati Yerusalemu Mpya itakapoonekana.
Tunaweza kudhani kwa usalama kwamba wakati huo hatutakuwa tumeuona mji huo, hata kama tutakuwa tumekuwa pamoja na Yesu mbinguni.
Utakuwa wakati wa kipekee sana, unaotupa jambo la kutazamia kwa hamu hata tunapoishi katika Ufalme wa Miaka 1,000
Katika uumbaji wa awali, Bwana pia aliandaa mji maalum kwa ajili ya wanadamu na kisha akamweka mwanadamu ndani yake
Ona kwamba katika uumbaji wa kwanza, mji huo uliumbwa duniani, kisha mwanadamu akawekwa ndani yake. Kwa maana hiyo, Adamu aliingia katika makao ambayo Mungu alikuwa amemwandalia.
Lakini katika Mbingu Mpya na Nchi Mpya, hali ni tofauti. Sisi tutakuwa tayari duniani, na mji wenyewe utashuka kutoka mbinguni kuja kwetu.
Katika mstari wa 3-8, Yohana anasikia tangazo kwamba kuwasili kwa Yerusalemu Mpya kunamaanisha kwamba vitu vyote vimerejeshwa katika hali kamilifu.
Athari zote mbaya za dhambi ya Adamu na laana zinazotokana nazo sasa zimerekebishwa na kurejeshwa.
Hiyo ndiyo sababu tunaendelea kuona uhusiano unaorudiwa kati ya Mwanzo sura ya 1 na ya 2 na sura hizi mbili za mwisho za Ufunuo.
Kwanza, katika mstari wa 3 Yohana anasema kwamba Mungu wa Utatu atakaa tena pamoja na wanadamu.
Kwa mara ya kwanza tangu bustani ya Edeni, Baba atakaa duniani
Tutakaa na Mungu kama Adamu alivyokuwa akiishi pamoja naye hapo mwanzo.
Pili, uumbaji wote utakuwa umetakaswa kutokana na dhambi na matokeo yake yote...hakutakuwa tena na alama zozote za dhambi.
Hakutakuwa na machozi, wala mauti, wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu. Mambo hayo yote yalikuja kwa sababu ya dhambi; hayakuwa sehemu ya uumbaji mkamilifu wa Mungu.
Dhambi ndiyo iliyomharibu mwanadamu na kuleta laana juu ya dunia na juu ya uumbaji wote.
Chanzo cha uasi na dhambi kinapatikana kwa Adamu, na hata kabla yake kwa Shetani.
Lakini hayo yote yatakuwa yamepita, na Bwana atakuwa ameyarekebisha kikamilifu.
Akiendeleza na kuimarisha taswira hii ya kurejeshwa kwa mambo yote katika ukamilifu wake, Yesu anatukumbusha katika mstari wa 5-6 kwamba anafanya vitu vyote kuwa vipya kama alivyoahidi kufanya.
Naye ndiye Alfa na Omega, mwanzo na mwisho
Kumbuka hapo mwanzo alikuwapo Neno, yaani Yesu Kristo, na kwa kupitia kwake (huyo Neno) mbingu na dunia ziliumbwa.
Na sasa, mwishoni mwa historia, Yesu anafanya uumbaji mpya tena. Kwa hiyo, kweli yeye ndiye Mwanzo wa uumbaji na pia Mwisho wake.
Na Yesu anaongeza kuwa yeye pia ndiye chemchemi ya uzima na haki iletayo uzima.
Ufunguo wa kushiriki utukufu huu wote ni kumwamini Alfa na Omega.
Ikiwa una kiu ya maji ya uzima—yanayoashiria kazi ya Roho atoaye uzima—basi Yesu ndiye anayekutosheleza.
Na wale wanaoshinda dhambi na mauti na adui na maisha haya maovu ni wale wanaoweka imani yao katika Yesu
Tunapofika mwisho wa kitabu hiki na mwisho wa Biblia, tunaona mwaliko wa kumwamini Yesu na kupokea wokovu ukirudiwa mara kwa mara.
Na hivyo ndivyo tungetarajia, kwa sababu hadithi hii ipo katika Biblia yetu si tu kwa ajili ya kuwatia moyo waumini kuhusu mustakabali wao.
Iko hapa kumshawishi asiyeamini amtafute Yesu wakati bado ana nafasi, na hivyo hoja hiyo itarudiwa katika sura ya 21 na 22.
Hata hivyo, kutakuwa na wengi watakaoendelea kusisitiza kuishi mbali na Mungu katika maisha haya, na kwa sababu hiyo watatumia umilele wote wakiwa wametengwa naye.
Na katika mst.8 Yohana anatoa orodha ya dhambi zinazowakilisha ama kuonyesha mtindo wa maisha wa mtu asiyeamini.
Orodha hii ya dhambi si ya wasioamini pekee, kwa maana hata sisi tunaweza kuwa tulifanya baadhi yake zamani, au hata bado tukapambana na baadhi yake sasa.
Hoja ni kwamba matendo hayo ni matunda ya kawaida ya kutokuamini, ilhali kwa waamini ni matendo yasiyopatana na asili yao mpya.
Inawezekana mwamini akaanguka katika baadhi ya dhambi hizo, lakini kufanya hivyo kunapingana na utu wake mpya ndani ya Kristo; kwa mtu asiyeamini, ndilo jambo linalolingana na asili yake.
Muhimu zaidi, katika siku hiyo, wasioamini ndio pekee watakaokuwa wakifanya mambo hayo, kwa sababu dhambi zote za watakatifu zitakuwa zimeondolewa kabisa.
Kwa hiyo, itakuwa kweli kusema kwamba wale wanaoendelea kuishi kwa namna hiyo ndio wanaokwenda kwenye adhabu ya milele.
Kwa maana tabia hizi zitakuwa za kipekee kwa kundi hili, na kama tulivyoona tayari, watapata kifo cha pili
Kigezo cha mwisho cha kutengwa si orodha ya dhambi zao peke yake, bali ni kwamba hawakumwamini Kristo. Kwa hiyo, wataingia katika Ziwa la Moto..
Kwa hiyo baada ya mji wa Yerusalemu Mpya kushuka kutoka mbinguni, sisi tuliopokea neema ya Mungu katika Kristo tutaingia katika mji huo, kama kitabu cha Waebrania kinavyoahidi.
Kulingana na Waebrania, mji huo utakuwa makao ya makundi kadhaa ya Uumbaji (yaani makundi mbalimbali ya viumbe wa Mungu.)
Kwanza kabisa, Mungu katika utimilifu wa Uungu wake atakaa ndani ya mji huo.
Pili, jeshi lote la malaika litaishi humo
Kisha kutakuwa na kusanyiko la wazaliwa wa kwanza, yaani Kanisa—Bibi-arusi wa Kristo wa Agano Jipya.
Hatimaye, kutakuwepo roho za wenye haki waliokamilishwa, yaani waamini wengine wote ambao Mungu amewakamilisha.
Hakika huo utakuwa ujirani wa kipekee sana, unaozidi kwa mbali hadhi ya eneo lolote la kifahari ambalo mtu anaweza kujivunia katika ulimwengu wa sasa.
Baada ya hayo, Yohana anatupa maelezo mafupi kuhusu mji huo, na kwa kuwa Maandiko hayatupi sehemu nyingine nyingi za kuulinganisha au kuufafanua zaidi, tutayapokea maelezo hayo kama yalivyoandikwa.